AfyaMtandao

CSSC yakabidhi Jengo na vifaa tiba hospitali ya St. Francis Kwamkono

Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (CSSC), imejenga jengo la upasuaji, uzio wa kuzunguka hospitali, sehemu ya kufulia na kuanikia nguo, Maliwato na kuweka mashine ya kuteketezea takataka katika hospitali ya St. Francis iliyopo katika kijiji cha Kwamkono, tarafa ya Sindeni inayomilikiwa na Kanisa la Anglicana,  wilayani Handeni mkoani Tanga,  vyote vikiwa na thamani ya Sh. 995 millioni.


Mbali na ujenzi huo ambao umefanyika kwa ufadhili wa Serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW), pia hospitali hiyo imekabidhiwa vifaa mbalimbali vya upasuaji.


Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi jengo hilo wilayani Handeni,  Naibu Waziri wa Afya na ustawi wa Jamii, Dkt. Seif  Rashid,  aliipongeza serikali ya Ujerumani iliyofadhili ujenzi huo,  KfW na wasimamizi wa mradi huo CSSC.
Dkt. Seif alibainisha kuwa huo ni mchango mkubwa katika kuboresha upatikanaji wa Huduma za afya hapa nchini, tofauti na misaada mingine, akionyesha kuwa mchango, huo umelenga kuboresha maisha ya Watanzania,  kwani bila huduma bora za afya na elimu hakuna maendeleo ya kweli.


Aidha Dkt. Seif ameelezea kuwa Serikali imeendelea kudumisha ushirikiano na sekta binafsi yakiwemo mashirikaya dini  ili kuwezesha sekta hizo kuwa na mazingira yanayoiwezesha ukamilifu katika utoaji wa Huduma za afya.
Meneja Mradi kutoka CSSC, Grace Mwang’onda, anasema ujenzi wa jengo hilo ni sehemu ya mradi mkubwa wa kusaidia sekta ya afya ambao unafadhiliwa na Serikali ya Ujerumani,na mradi huo ulianza kutekelezwa mwaka  2009  na kukamilika mwezi Desemba, 2013. Anatoa rai kwa wahusika kulitunza Jengo hilo ili liendelee kubaki katika hadhi yake.


Bunge  wa  jimbo  la  Handeni,  Dkt . Abdallah Kigoda,  alisema  wilaya  hiyo  ina asilimia 33 ya  wakazi  wote wa Tanga; hivyo  hospitali hiyo  ni  muhimu ikaboreshwa  kwani  inategemewa  na  wananchi  wengi.Mkuu wa  Wilaya  ya Handeni,  Muhingo  Rweyemamu,  alipongeza  wafadhili kwa  kufanikisha  jengo  hilo  la upasuaji  na  kuongeza kuwa   uongozi  wa   mkoa  unaipa nafasi  kubwa hospitali hiyo.


Naye  Mganga  Mfawidhi  wa hospitali hiyo,  Dkt. George Chausa,  alisema hospitali hiyo ambayo ilianzishwa mwaka 1917 inakabiliwa na uchakavu wa majengo na upungufu wa vifaa tiba. Alisema hospitali hiyo  ni miongoni mwa hospitali mbili ambazo zinategemewa na wananchi wa wilaya hiyo.

Views: 382

Add a Comment

You need to be a member of AfyaMtandao to add comments!

Join AfyaMtandao

© 2024   Created by sona.   Powered by

Badges  |  Report an Issue  |  Terms of Service